Mwanamke aliyekamatwa akiiba petroli (ambayo hapa Marekani huitwa gesi) ya thamani ya dola 4 na senti 52, aliamriwa na mahakama kusimama nje ya kituo hicho cha petroli na bango kubwa mbele ya kifua chake lisemalo: NILIKAMATWA NIKIIBA PETROLI.
Watu walijaa hapo kituoni kumuona na wengine walipeleka watoto wao ili wajifunze ubaya wa wizi. Bonyeza hapa utazame picha yake na habari yenyewe.
July 2004
Sat 31 Jul 2004
Thu 29 Jul 2004
Inaelekea bado tatizo la tovuti/ webu ambako ndiko ninahifadhi makala zangu liko pale pale. Ninaomba samahani tena. Nimepata barua pepe za wale wanaolalamika kuwa wanapokongoli ziliko makala hawapati kitu. Ni kweli. Kuna tatizo. Ninajitahidi kusawazisha.
Wed 28 Jul 2004
Jina la Mungu limetumiwa miaka nenda rudi kuhalalisha unyama. Mwizi wa kura George Bush na wahafidhina wenzake wanadai kuwa vita wanavyoviongoza dhidi ya “ugaidi” ni vita ya wenye Mungu wa kweli dhidi ya wafuasi wa shetani. Makundi yanayojiita kuwa ni ya kiislamu nayo yanafanya unyama dhidi ya wengi wasio na hatia kwa madai kuwa wanapigana vita vya kidini. Wanampigania Mungu wa kweli! Mwanazuoni mmoja, jina limenitoka, aliwahi kusema kuwa dunia ina dini za kutosha kutufanya tuuane, tugombane, na kuchukiana lakini hakuna dini za kutufanya tuishi kama ndugu.
Tazama picha hii ya unyama usio na mfano uliofanya dhidi ya Mmarekani Nick Berg. Napenda kukutaarifu kuwa picha hii, hasa mwishoni, inatisha na kuchafua roho kabisa. Kama una roho nyepesi nakushauri usiitazame. Kongoli hapa uione.
Tue 27 Jul 2004
Kwanza kabisa poleni. Kisha karibuni ndani! Toka kupambana na Mwalimu Sango hadi kupambana na Rais Kichaka!
Mon 26 Jul 2004
Imeelezwa kuwa Saddam Hussein anatumia muda wake jela kuandika mashairi. Moja ya mashairi yake linamhusu dikteta mwenzake aitwaye George Bush. Pia anapenda sana kutengeneza bustani. Taarifa zinasema kuwa anapenda kula mkate wa Kimarekani uitwao Muffins, na biskuti. Kongoli hapa usome habari nzima. Sijui kama unajua kuwa Saddam ni mtunzi pia wa vitabu. Ameshaandika vitabu vitatu: Zabibah and the King, The Fortified Castle and Men and the City, na Be Gone Demons! Vitabu hivi vilichapwa bila jina la mtunzi. Kongoli hapa usome zaidi.
Mon 26 Jul 2004
Tuenzi vitendawili.
Nani anaweza kutegua kitendawili hili?
Kitendawili…
Msichana wangu amejishika kiuno.
Una jibu? Niandikie.
Mon 26 Jul 2004
Ninapitia vitabu vyangu vya kumbukumbu nilizoandika nikiwa Tanzania. Hii ni sehemu ndogo ya mambo niliyoandika katika pilikapilika za kwenye daladala katika jiji la Dar Es Salaam. Ni kati ya mwaka 1999-2001.
Kondakta: Kaa mkao wa pesa.
Abiria: Si tumetosha? Twende basi!
Mon 26 Jul 2004
Kutakuwa na mabadiliko ya muundo na rangi ya blogu hii siku za karibuni. Mpangilio wa kila kitu utakuwa tofauti. Ila blogu itakuwa “rafiki wa watumiaji” kuliko ilivyo hivi sasa.
Fri 23 Jul 2004
Bado mjadala huu haujatuama. Je wanablogu (bloggers) ni waandishi wa habari? Je blogu ni uandishi? Waandishi, wanasiasa, watengeneza sera, wanataaluma, n.k. wana mawazo tofauti juu ya blogu. Wako wanaosema kuwa wanablogu (bloggers) ni aina fulani ya waandishi. Wengine wanasema hapana. Lakini kukubaliwa kwa wanablogu kuhudhuria mkutano wa chama cha Demokrasia cha hapa Marikani, ambao utampitisha John Kerry na John Edwards kuwa wagombea Urais na mgombea mwenza, kumechukuliwa kama ni moja ya hatua ambazo zinawapa wanablogu hadhi ya uandishi.
Fri 23 Jul 2004
Kama hujatazama sinema mpya ya Michael Moore : Fahrenheit 911, tafadhali sana nenda kaitazame. Pia tazama filamu zake nyingine hasa Bowling For Columbine na Roger and Me. Nenda kaitazame, utakuja kuniambia! Wale walioko Tanzania, kuna kundi la vijana wenye mwamko wa kimapinduzi ambao watakuwa na kopi yake siku za karibuni. Nitatoa maelezo ya jinsi ya kuwapata.
Fri 23 Jul 2004
“Sitaomba msamaha.” Haya ni maneno ya Rais wa Ufilipino, mwanamama Gloria Arroyo, kufuatia kuondoa majeshi ya nchi yake toka Iraki ili kuokoa maisha ya Angelo de la Cruz aliyekuwa ameshikiliwa mateka huko Iraki. Arroyo anasema kuwa Angelo ana familia ya watoto tisa wanaomhitaji hivyo uhai wake ndio kipaumbele cha nchi yake. Serikali ya Rais Kichaka (Bush) imetoa malalamiko juu ya hatua hiyo.
Tujiulize: Hivi binti yake Bush angekuwa ameshikiliwa na hao jamaa na wakiwa wanatishia kumkata kichwa, Bush angesema, “Potelea mbali. Wamuue. Siwezi kutimiza masharti ya magaidi. Nafuu mtoto wangu auawe kikatili kuliko kuwasikiliza. ” Angethubutu kusema hivyo? Thubutu!
Fri 23 Jul 2004
Ndugu zanguni, kuna tatizo kidogo kwenye “link” za makala zangu. Ninarekebisha. Kwahiyo baada ya muda mfupi mtaweza kupata makala ninazotoa kwenye gazeti la Mwananchi kila jumapili. Na pia makala nyingine nilizoandika huko nyuma kwenye magazeti mengine. Na tafsiri ya zile nilizoandika kwa kiswahili. Ninaomba mniwie radhi kwa usumbufu. Makala unayoweza kuipata ni moja iitwayo BABU SEYA. Hii ilitoka jumapili mbili zilizopita.
Fri 23 Jul 2004
Baada ya wapinzani kumtoa madarakani dikteta aliyekalia kiti toka mwaka 1979, Mzee Moi, wapinzani wa Tanzania walitumia nafasi hiyo kuwataka wananchi wakatae chama tawala na kuleta mabadiliko. Kama Kenya ndio mfano ambao viongozi wa upinzani Tanzania wanataka wananchi wauige, basi huu ni mfano mbaya sana. Kenya inatupa fundisho moja kubwa sana. Vyama vya siasa vinaongozwa na binadamu. Viwe ni vyama vya upinzania au chama tawala. Wezi wa chama cha KANU hawakuwa wakiiba eti kwakuwa wao ni wanachama wa KANU. Waliiba kwa kuwa ni wanadamu ambao hawana maadili na utu. Ubinadamu wa viongozi wa upinzania hauna tofauti na ubinadamu wa viongozi wa chama tawala. Tunaona jinsi ambavyo viongozi waliokuwa wakidai kuwa katiba ya Kenya ibadilishwe, sasa wameingia madarakani wamebadili msimamo. Tumeona kashfa za rushwa zinawaandama kila kukicha. Leo hii gazeti la Daily Nation lina habari hii ya Waziri wa Uchukuzi ambaye inaelekea kapewa kitu kidogo na Wachina. Umeusikia wimbo wa Wainaina uitwao Kenya Nchi ya Kitu Kidogo? Anasema, “askari kama unataka chai nenda Limuru: Limiru inalimwa chai. Kenya ni nchi ya kitu kidogo wakati wa “baba” Moi. Ni nchi ya kitu kidogo wakati wa Mzee Kibaki. Halafu unaona nchi zetu za Afrika, badala ya ku-recycle takataka, tuna-recycle watawala.
Fri 23 Jul 2004
Wabunge wenye siasa za kihafidhina wameshindwa kupitisha sheria ambayo ingeifanya katiba ibadilishwe ili kutamka kuwa ndoa ni kati ya mwaume na mwanamke! Rais Bush na chama cha Republican wamekuwa mstari wa mbele kutafuta njia ya kuzuia kisheria kasi ya ndoa za wanaume kwa wanaume na wanawake kwa wanawake. Swali ambalo Bush na wenzake wanashindwa kujibu hadi hivi sasa ni hili: kwanini wanataka kubadili katiba kwa kutumia imani zao za kidini?
Bush na wenzake wanadai kuwa ndoa mwanaume na mwanamke ndio mapenzi ya Mungu. Sasa kama je mtu hamwamini huyo Mungu wao? Hili suala kwa kifupi ni gumu sana. Huko Afrika Kusini kipindi cha luninga cha Yizo Yizo kimeonyesha wanaume wawili wakipigana busu kwa mapenzi na mahaba yasiyo na kifani. Ni mara ya kwanza kwa luninga nchini humo kuonyesha picha ya namna hii. Afrika Kusini ndio nchi pekee Afrika hivi sasa ambayo katiba yake inatoa haki kwa watu wa jinsia moja kuwa na mahusiano ya kimapenzi.
Wed 21 Jul 2004
Jifunze kiswahili:
Genetic engineering= uhandisi wa maumbile
Biodiversity= bioanuai
Cloning= kupachiza
Hacker= mchazaji
DNA= shanga za urathi
Stem cells= seli asili
Wed 21 Jul 2004
Ndugu yangu uliyetuma maoni yako kwa jina la CRITIC, tafadhali sana nitumie anuani yako. Nadhani uko New York. Umezungumzia juu ya Taifa la Waislamu. Ningependa kuwa na anuani yako ili tuendeleze mjadala. Pia kuhusu blog kwa kiswahili, nadhani itaitwa blogu. Kwahiyo weblog itakuwa webulogu au tovutiblogu.
Wed 21 Jul 2004
Narudia kuweka tena sehemu ya shairi langu liitwalo “Utamaduni Msalabani.” Wengi wametaka niweke sehemu nzima. NItafanya hivyo karibuni. NItarudia sehemu niliyoweka mwezi uliopita. Nataka usome na utafakari sana mistari hii michache.
Utamaduni Msalabani
Kura twapiga,
Sadaka twatoa,
Kodi twalipa,
swala twasali,
Walalanjaa Cha moto,
mbona
Bado twakiona?
Demokrasia ghasia
Mafukara twauziwa,
Jehanamu ya moto
Masikini twatishiwa,
Wa kusema wamesema
Wa kusikia ni viziwi,
Hivi chukua chako mapema
Ni azimio la wapi?
- Dar Es Salaam, Tanzania 2003
Tue 20 Jul 2004
Bado ninaendelea kukumbana na watu wanaohubiri kuwa Yesu yu karibu kuja. Mimi siwaelewi kabisa. Ninavyoelewa mimi ni kuwa Yesu yu karibu aondoke. Yuko nasi toka siku nyingi ila hatujui. Sijui tunasubiri ashuke toka mawinguni. Unajua asilimia 90 ya mambo ambayo Yesu aliyasema yalikuwa ni mafumbo. Usipoweza kufumbua, utabaki ukimsubiri. Kwanza watu wengi wanaomhubiri Yesu, hawamfahamu Yesu sawasawa. Yesu ninayemjua mimi akija leo hii hatakwenda kanisani wala msikitini. Akafanye nini? Watu wake hawako huko! Wakristo na waislamu wanabaki kushikana makoo, “Yesu hakusulubiwa,” “Yesu mwana wa Mungu,” “Yesu alikuwa ni muislamu,” “Yesu alimwaga damu ya ukombozi.” Yesu, Yesu, Yesu…. Akija wala hatapoteza muda huko. Atawaacha waendelee na ibada na swala zao na mihadhara na ma-crusade.
Kila mara ninaahirisha makala ninayotaka kuandika juu ya hili jambo. Ninahitaji makala ili nichambue vizuri na kufafanua nina maana gani ninaposema kuwa Yesu karibu aondoke. Na kuwa Yesu akitokea Tanzania leo hii hatakwenda kanisani wala msikitini. Watamsikia kwenye “bomba”!
Sun 18 Jul 2004
SAHAU KABLA YA ALFAJIRI !
La mgambo limelia
wa kusikia wamesikia,
kama ni Ukimwi, haya
kama ni wanawake, haya
kama ni utandawizi, haya
kama ni watoto, haya,
ili mradi una ishu
inayokubalika
kwa wafadhili.
Usijali.
Mikutano
warsha
makongamano
semina
vikao
utafiti
mafunzo….
Tukutane
tuongee
tulalamike
tuonye
tushauri
tukemee
tunywe chai, kahawa
mlo wa mchana
mshiko tushike
picha tupige
tuondoke
tusahau yote kabla ya alfajiri.
Mla kesho ni mla leo.
- July 18, 2004, Toledo, OH
Tue 13 Jul 2004
Mwaka 1999 Ikaweba Bunting alifanya mahojiano na Mwalimu Nyerere. Mahojiano hayo yalitolewa katika gazeti la New Internationalist. Nimependa sana jibu lake hili. Soma mwenyewe:
I was in Washington last year. At the World Bank the first question they asked me was `how did you fail?’ I responded that we took over a country with 85 per cent of its adult population illiterate. The British ruled us for 43 years. When they left, there were 2 trained engineers and 12 doctors. This is the country we inherited.
When I stepped down there was 91-per-cent literacy and nearly every child was in school. We trained thousands of engineers and doctors and teachers.
In 1988 Tanzania’s per-capita income was $280. Now, in 1998, it is $140. So I asked the World Bank people what went wrong. Because for the last ten years Tanzania has been signing on the dotted line and doing everything the IMF and the World Bank wanted. Enrolment in school has plummeted to 63 per cent and conditions in health and other social services have deteriorated. I asked them again: `what went wrong?’ These people just sat there looking at me. Then they asked what could they do? I told them have some humility. Humility - they are so arrogant!
Ndio Mwalimu huyo. Ukitaka mahojiano kamili kongoli hapa.
Ukitaka kusikiliza hotuba za Mwalimu Nyerere nenda hapa.



