May 2005
Tue 31 May 2005
Mon 30 May 2005
Paula LeDieu, aliyewahi kuwa mkurugenzi wa idara ya nyaraka huru za shirika la habari la BBC, aliongea jioni ya tarehe 26 katika mkutano wa Commons-Sense. Alitumia kama dakika ishirini hivi kuzungumzia uamuzi wa shirika hilo kutumia modeli ya hatimiliki ya Creative Commons. Mradi uitwao The Creative Archive unaruhusu wakazi wa Uingereza (kwakuwa kodi yao ndio inaendesha shirika hili) kutumia kwa njia zozote zile (isipokuwa kibiashara) nyaraka zote za shirika hilo. Mradi huu ulianza rasmi mwaka jana.
Kwakuwa BBC ilianzishwa mwaka 1922, rundo la nyaraka ambazo imehifadhi ni kubwa kiasi ambacho inakupasa ukae mbele ya luninga yako ukitazama bila kuzima kwa miaka 68, masaa 24 kwa siku! Utaweza?
Mon 30 May 2005
Nimewasili Babiloni. Safari nzima nilikuwa najiuliza, “Hivi nitablogu nini na nini nitaacha?” Kwanza hata pa kuanzia sijiu. Nimeamua kuwa nitakuwa nablogu kila siku mambo kadhaa yaliyotokana na mkutano wa Commons-sense; mambo niliyojifunza, watu niliokutana nao, miradi mbalimbali inayotumia zana mpya za mawasiliano Afrika, niliyoona katika jiji la Egoli/Jozi (majina ya jiji la Johannersburg), mapana na marefu ya dhana hii ya “creative commons” (bado natafuta tafsiri yake sahihi ya Kiswahili), n.k.
Ndio nimeamka nataka kunywa chai. Ningependa kwa sasa utazame video hii ya mahojiano niliyofanya na New Media Lab ya chuo kikuu cha Rhodes. Bonyeza hapa uitazame.
Sat 28 May 2005
Mshikaji wangu, Donald (jamaa nikitaka kumwelezea sijui nitaanzia wapi), ananizungusha katika jiji la Egoli. Tumetoka katika mahakama ya katiba ambayo ilikuwa ni gereza liitwalo Old Fort. Nimepita kwenye mgahawa huu kutazama jambo fulani kwenye mtandao. Picha na yote yanayohusu mkutano wa Commons-Sense ni mpaka nitakapowasilia Babiloni kwa Joji Kichaka mwizi wa kura. Ninaondoka leo usiku.
Uhuru!
Fri 27 May 2005
Thu 26 May 2005
Wed 25 May 2005
Kwa wale wasiofahamu, ninahudhuria mkutano unaoitwa Commons-Sense ulioandaliwa na chuo kikuu cha Wits, Creative Commons (Afrika Kusini), na Links. Mkutano huo unafanyika hapa katika jiji la Egoli ( jina la Kizulu la jiji la Johannersburg). Shughuli rasmi zitaanza leo jioni kwa tafrija ya mkia wa jogoo (kwa kiingereza wanaita “cock tail”). Tayari nimekutana na watu wawili ambao nao wanahudhuria mkutano huu. Dada mmoja toka Kenya na mwingine toka Marekani.
Nenda hapa kwa taarifa zaidi juu ya mkutano huu.
Jana usiku, ingawa nilikuwa nimechoka, sikujisikia kulala. Nilishuka chini (ninakaa hapa) kwenda kuongea na waswahili wenzangu ambao kazi zao ni ulinzi, ufagizi, kufungua milango, n,k. Tsedu ni mlinzi wa usiku hotelini hapa. Anaishi kitongoji cha Alexandra. Tsedu ni rasta: anamuenzi Mfalme wa Wafalme, Simba wa kabila la Yuda Haile Selassie I, Jah! Rastafari!
Tsedu alinivunja mbavu. Baada ya kuniambia kuwa yeye ni rasta na anapenda sana kusikiliza muziki wa hisia na mafunzo, Rege, nilimuuliza kama anampenda Lucky Dube. Akanitazama kwa mshangao na kusema, “Dube hapigi rege. Ile sio rege!” Tsedu anawasikiliza wanamuziki kama Culture, Burning Spear, Bob Marley, Mutabaruka (yule mshairi anayetembea pekupeku), Luciano, n.k. “Rege ni mafunzo, ni tenzi za rohoni, ni mashairi ya kiroho…” Tsedu ananiambia.
Karibu kila wimbo niliomtajia wa wanamuziki anaowasikiliza, alikuwa amekariri maneno yake na hata ufafanuzi wa jinsi ujumbe wa nyimbo hizo unavyoendana na hali ya kisiasa, kiuchumi, na kiutamaduni duniani hivi sasa. Nilipomtajia wimbo wa Burning Spear uitwao “Days of slavery.” Alitabasamu huku akitikisa kichwa. Kisha akaanza kuuimba. “Watu wengi wanaposikiliza huu wimbo wanafikiria mambo yaliyotokea miaka mingi iliyopita. Hapa Afrika Kusini utumwa anaozungumzia Burning Spear upo hadi leo.”
Tulipiga gumzo na Tsedu kwa masaa kadhaa…nadhani nilienda kulala saa tisa. Nilipomtaja Steve Bantu Biko, Tsedu alitazama chini, uso wake ukajaa huzuni. Alikaa kimya kwa muda kisha akasema, “Black consciousness.” Black Consciousness ni jina la falsafa na itikadi aliyokuwa akihubiri mwanamapinduzi Biko. Baada ya muda kidogo alinieleza kwa kina jinsi Biko alivyouawa kinyama. Alivyoburuzwa akiwa amening’inizwa nyuma ya gari katika barabara ya kokoto. Uchi wa myama. Alipomaliza kunieleza kwa undani na hisia kali niligundua kuwa sikuwa ninafahamu kwa kina yaliyotokea siku za mwisho wa uhai wake. Maelezo yake yalinitia hasira na huzuni kwa wakati mmoja. Hadi sasa bado kuna donge limekwama kooni.
Nilipomuuliza Tsedu juu ya kitongoji anachoishi, visa alinieleza visa ambavyo vimenijaza huzuni kubwa. Anasema kuwa maisha wanayoishi Waafrika katika vitongoji mbalimbali nchini humu hayana thamani yoyote. Vifo kutokana na ukimwi, ujambazi wa kutumia silaha vimekuwa ni kitu cha kawaida. “Nikiwa nyumbani nikasikia mlio wa risasi huwa ninaendelea na shughuli zangu. Hata watoto wangu wamezoea. Kila mtu kazoea. Hakuna anayeshtuka. Tumekuwa sugu. Tumekuwa viziwi. Tumekuwa vipofu. Hii ndio njia pekee ya kuendelea kuwa na akili timamu. Bila hivyo utarukwa na akili au utakata tamaa na kujiua. Anasema majambazi katika vitongoji vya weusi wamefika hatua ambayo hakuna kinachowazuia kupora mtu yeyote na saa yeyote. “Majambazi wanampora mtu pembeni yako, unatazama na kuendelea na shughuli zako.” Ananiambia.
Anasema kuwa siku moja aliporwa simu ya mkono. Kawaida akiwa vitongojini hapendi kutumia simu yake. Siku hiyo alisahau kuizima. Akiwa anapita mtaani, simu ikalia. Jamaa watatu wakamfuata, mmoja wao akamwambia, “Pokea hiyo simu. Ukishamaliza kuongea tupe simu yetu.” Wakati wanamwambia hivyo mmoja wao alikuwa amechomoa bastola.
Nitakutana na Tsedu leo usiku baada ya ufunguzi rasmi wa mkutano na tafrija ya mkia wa jogoo. Usisahau kutembelea tovuti ya mkutano huu. Nitakuwa ninawapa taarifa mbalimbali kadri mkutano unavyoendelea. Ninakwenda kutembea mjini hadi jioni. Sijui nikanunue bastola…maana nataka kwenda ile mitaa ninayoambiwa kuwa nisithubutu kupeleka unyayo. Huko ndio ninataka kwenda. Niombeeni!!!!
Sobonana futhi (tutaonana baadaye kwa Kizulu).
Sun 22 May 2005
Nilikosea kiungo cha mviringo wa blogu za Kiswahili. Mviringo huu hapa.
Tue 17 May 2005
Kwanza nilitangaza blogu ya Kishona. Hapa. Kisha nikatangaza blogu ya Kichagga. Hapa. Sasa rafiki yangu, Mokhtar, toka Morocco ameanza kublogu kwa lugha ya Kiberber, Tamazeight. Mokthar ni anafundisha Kiarabu katika chuo hiki. Blogu yake hapa. Nina mambo mengi ya kuandika na kutundika lakini muda umekuwa mdogo. Jumamosi ndio siku ninaongea katika mkutano wa Afrogeeks kuhusu blogu za Kiswahili na jumatatu ninaondoka kwenda Afrika Kusini kwenye mkutano wa Commons-Sense.
Mon 16 May 2005
Baada ya kuanza kufumuka blogu za Kiswahili, mwanadada toka kule kwa Mangi Horombo, chini ya mlima wa Ruwa (Kilimanjaro), amekuja na blogu kwa lugha ya Kichagga. Mtembelee Mtafiti na blogu yake hapa. Mtafiti hivi sasa yuko masomoni nchini Marekani ila anaendelea kuenzi utamaduni wake.
Mon 16 May 2005
Shukrani za dhati zinamwendea ndugu yetu Maitha. Ametupatia mviringo wa blogu za Kiswahili. Tembelkea mviringo huo hapa.
Fri 13 May 2005
Dakika hii ninavyoandika ninasubiri dakika chache kabla ya kufanya mahojiano kuhusu blogu na redio ya Open Source. Nenda hapa.
Tue 10 May 2005
Tue 10 May 2005
Haya. Kuna makala nne kabambe za Padri Karugendo. Zinaitwa: Tuacheni Tutetee Matumizi ya Kondomu, Tumwogope Mungu kwa Matendo Yetu Yote Kila Siku na Kila Wakati, Papa Benedikto ni Rafiki wa Tanzania, na Elimu, Vijana, na Uchumi. Bonyeza juu ya makala unayotaka kuisoma. Kumbuka makala zake za nyuma ziko katika kona yake, Kalamu ya Padri Karugendo chini ya makala zangu naFreddy Macha.
Sun 8 May 2005
Sun 8 May 2005
Nipe Aya! ni moja ya makala mbili mpya ambazo nimepandisha hapa ndani. Kaba ya kusoma makala hizi ni vyema ukasoma kwanza makala ya Wazee Afrika ni Vyuo Vikuu ambayo iko katika kona ya makala zangu, chini ya picha yangu. Makala ya kwanza leo inaitwa: Soma Anga, Mawingu, na Nyota Kama Kitabu. Bonyeza hapa. Ya pili ndio hii ya Nipe Aya! Bonyeza hapa.
Sun 8 May 2005
Sat 7 May 2005
Niliutaja huu mkutano siku za nyuma. Usiache kuufuatilia. Ni ule mkutano wa Commons-Sense huko Afrika Kusini. Nenda hapa. Pia kama ni mwanablogu au mtafiti wa masuala ya zana mpya za mawasiliano na habari unaweza kupewa skolashipu. Fanya hima. Nenda hapa kuna fomu fulani ya kujaza.
Thu 5 May 2005
Tanga kunani? Kuna wimbo ule wanasema kuwa Tanga watu huoga na maji yenye viungo kama mdalasini na iliki! Na Dokta Remmy, katika kibao cha Mariamu anasema, “Waja leo, warudi leo, Tanga mbali…” Sasa kaingia binti kutoka Tanga katika ulimwengu wa blogu za Kiswahili. Blogu yake inaitwa Wanawake na Maendeleo. Nenda hapa umsome na kumkaribisha.
Thu 5 May 2005
Kuna wakati unasoma jambo, linakuingia hasa hadi unaamua kuacha kusoma na kwenda kunywa maji, kujisaidia, kujinyoosha, kutengeneza chai, kisha unarudi tena kusoma. Ndio imenitokea leo nilipotembelea blogu ya Mwandani. Nimekwenda hapo nikakuta amemnukuu shujaa Marcus Mosiah Garvey. Nimechukua nukuu hiyo. Hii hapa:
Ni wachache tu kati yetu, ambao wanaelewa ni kitu gani kinachomfanya mtu awe mtu!Namaanisha -Mtu asiyeweza kufa moyo; mtu asiyeweza kukata tamaa;
Mtu asiyetegemea wengine wamfanyie yale anayoweza kuyafanya yeye mwenyewe;
Mtu asiyemlaumu Mungu, asiyelaumu mazingira;
mtu asiyelaumu ‘bahati mbaya’ kwa hali yake kimaisha;
Bali yule mtu awezaye kutoka na kujitengenezea mazingira yanayomwezesha kuishi.
Kweli nawaambia, ikiwa sisi watu weusi milioni mia nne tungekuwa tunajitambua,
Na tungetambua kwamba ndani yetu tunao uwezo na haki,
Na kwamba tunayo mamlaka kamili,
Ama kwa hakika nawaambieni, mnamo masaa ishirini na nne tu yajayo tungekuwa na taifa jipya,
Tungekuwa na dola iliyosimama kisawasawa,
Si kutokana na matakwa ya watu wengine wowote ya kutaka kutuona tunatengenekewa,
Bali kutokana na moyo wetu dhabiti wa kutakaka kujiinua,bila kujali watu wengine humu duniani wanatufikiriaje.
-Marcus Mosiah Garvey



