September 2005
Monthly Archive
Wed 28 Sep 2005
Na , Maudhui: Uncategorized
Toa Maoni
Ile kamusi elezo ya Kiswahili (Kiswahili wikipedia) ambayo inaandikwa na kuhaririwa na mtu yeyote anayezungumza Kiswahili inahitaji msaada wako wewe mpenda lugha yetu tamu…kumbuka Shaban Robert na “titi la mama litamu ingawa la mbwa…” Kamusi hii ukilinganisha na kamusi elezo za lugha nyingine kama vile wikipedia ya kiingereza , kifaransa au Kidachi iko nyuma kidogo. Yeyote yule ambaye ana muda anaweza kushirika kuipanua kwa kufanya mambo kadhaa: kuandika makala mpya, kuhariri zilizopo, kuitangaza (hawa wanablogu wana nafasi ya kuitangaza), n.k. Ukienda hapa utapata taarifa zaidi juu ya mambo ya kufanya ili kuiboresha. Ukurasa mkuu wa wikipedia yetu huu hapa.
Tue 27 Sep 2005
Na , Maudhui: Uncategorized
Toa Maoni
Tue 27 Sep 2005
Na , Maudhui: Uncategorized
Toa Maoni
Niliandika muhtasari huu hivi majuzi kwa ajili ya blogu ya Sauti za Dunia (Global Voices) kuhusu mkutano niliohudhuria majuzi kule Helsinki, Ufini. Usome kwa kubonyeza hapa.
Tue 27 Sep 2005
Na , Maudhui: Uncategorized
Toa Maoni
Jalo karibu sana. Ni masika nyingi zimepita…karibu sana sana. Hapa ni sebuleni kwangu.
Zimepita siku nyingi. Miaka mingi. Toka pale namba saba (nadhani ilikuwa namba sana), kule darinini…
Hongera sana.
**Ujumbe huu ni wa mafumbo. Ni mtu mmoja tu atakayelewa na ndiye anayepaswa kuelewa.
Tue 27 Sep 2005
Na , Maudhui: Uncategorized
Toa Maoni
Nitakapomaliza mkutano wa We Media: Behold the Power of Us kule New York tarehe 5 mwezi ujao, nitaondoka nikikimbia nikikatiza “shotikati” moja ya kupitia kwenye mashamba ya mahindi kuelekea North Carolina kwa ajili ya mkutano mwingine mkubwa kuhusu zana mpya za mawasiliano (masuala ya blogu yakiwa yamepewa kipaumbele) utakaofanyika tarehe 7 na 8 mwezi ujao katika chuo kikuu cha A and T, North Carolina.
Mkutano huu utakaomshirikisha mwanablogu anayesukuma vuguvugu la kidemokrasia nchini Irani kwa kutumia blogu, Hoder,
unaitwa ConvergeSouth.
Kisha tarehe 19-22 mwezi Oktoba nitakuwa katika mji wa kizamani wa Camden katika jimbo la Maine kuhudhuria mkutano wa kila mwaka unaokutanisha watu toka sekta mbalimbali kujadili na kubadilishana mawazo juu ya teknolojia na mabadiliko ya jamii. Mkutano huu unaitwa Pop!Tech 2005.
Tue 27 Sep 2005
Na , Maudhui: Uncategorized
Toa Maoni [2]
Nadhani hadi “mwokozi” akija mara ya pili atatukuta wanadamu tuko kwenye mikutano. Wanadamu tunapenda sasa kukutana…na kuongea na kupanga mikakati. Bila kusahau kula na kunywa mvinyo.
Haya hekaheka za mikutano hazijaniisha. Tarehe tano mwezi ujao nitakuwa New York kwa mkutano wa siku moja ulioandaliwa na Kituo cha Habari cha Taasisi ya Habari ya Marekani (API) uitwao We Media: Behold the Power of Us.
Ninahudhuria mkutano huu wa siku moja kupitia udhamini wa Kituo cha Habari kwa watu 15. Orodha ya waliopata udhamini huo hii hapa:
* Nathalie Applewhite, Candidate, Master of International AffairsSchool of International and Public Affairs, Columbia University
* Anjali Arora, Freelance Consultant in Information Architecture /User Experience Design
* Dr. Ralph Braseth, Director of Student Media & Assistant Professorof Journalism, The University of Mississippi
* Kent Bye, Director, The Echo Chamber Project
* Andy Carvin, Director, Digital Divide Network, EDC Center for Media& Community
* John Mwendwa Gitari, Fanning Fellow, Kettering Foundation
* Timothy Karr, Campaign Director, Free Press
* Kathryn Kross, Deputy Director, Center for Public Integrity
* Katie Lips, Creative Technologist and Co-Founder, Kisky Netmedia
* Ndesanjo Macha, Blogger, Jikomboe and Digital Africa
* Ron Mwangaguhunga, Editor, The Corsair
* Steven C. Podd, Principal, Nesaquake Middle School
* John Schott, Chairman, Cinema & Media Studies, Carleton College
* Elina Shcop, Founder, Kaleidoscope of Living (KOL)
* Nichelle Stephens, Blogger, nichellenewsletter
Tue 27 Sep 2005
Na , Maudhui: Uncategorized
Toa Maoni
Mambo mengi yametokea na yanaendelea kutokea toka niandike mara ya mwisho. Yapo ambayo nisingependa yakupite. Kwanza kabisa leo hii kutakuwa mahojiano kati ya mkurugenzi wa masuala ya mtandao wa Wanahabari Wasio na Mipaka, Julien Pain, kuhusu kitabu kizuri sana walichokitoa kuhusu uanaharakati wa mtandaoni. Kitabu hiki ambacho ni kiongozi cha wanablogu na wanaharakati wa mtandaoni kinapatikana bure hapa. Mtu yeyote anaweza kushiriki kwenye mahojiano hayo ambayo yatafanyika kwa kutumia teknolojia ya Internet Relay Chat (IRC). Taarifa kamili kuhusu saa na jinsi ya kuingia kwenye mtandao huo wa IRC nenda hapa.
Rebecca MacKinnon amechambua kwa ufupi yaliyomo katika kiongozi hiki. Msome hapa.
Tue 27 Sep 2005
Na , Maudhui: Uncategorized
Toa Maoni
Baada ya kuondoka kwenye ule mkutano wa kuuziana maneno kama ilivyo mikutano mingi niliingia mitini kimya kimya. Nilikwenda mahala kwa mapumziko kisha nikaenda kwa Kichaka. Kisha nikaondoka tena, kimya kimya. Sasa niko mahala fulani ambapo sipendi kusema ni wapi! Lakini utashangaa…huenda niko jirani nawe. Huenda niko mtaa wa pili na hapo ulipo. Kwahiyo tukikutana barabarani, kijiweni, au mgahawani usije sema sikukwambia. Huenda niko Aruba. Au labda visiwa vya mtakatifu Helena. Au pengine niko pembeni ya kwa msikiti wa Kwa Mtoro jijini Dasalama. Au labda pembeni ya soko la Kiboriloni mjini Moshi. Au ufukweni mwa bahari Mambasa (yaani Mombasa). Au kwa Bibi Lizabeti. Au Trenchtown kwa Bob Malya, nchini Jamaika. Utajaza mwenyewe.
Nilipo ninavaa miwani nyeusi kila siku. Na kichwani kofia kubwa. Unaweza usinitambue. Jaribu kutafuta mtu mwenye miwani nyeusi ya ki-KGB na kofia kubwa ambaye anatembea na kompyuta ndogo ya mapajani akitafuta mawimbi ya mtandao usiwaya (wi-fi). Ni mimi.
Nina picha tulizopiga pale klabu ya Chelsea, jijini Helsinki. Hapa ndio wanapokutana Watanzania wanaoishi Helsinki. Basi wageni na wenyeji tulikutana hapo na kupiga picha. Kabla sijazitundika nitawauliza kwanza walioko kwenye picha kama ni sawa kuziweka hapa.
Sun 11 Sep 2005
Na , Maudhui: Uncategorized
Toa Maoni
Kati ya mijadala iliyokuwa mikali ni ule kuhusu rushwana maendeleo. Ilikubalika kuwa moja ya chanzo kikubwa cha rushwa katika jamii mbalimbali duniani ni rushwa. Ami Mpungwe wa Namitech East Africa alidai kuwa tofauti na mtazamo wa wengi rushwa sio tatizo la nchi masikini tu. “Tatizo ni kuwa rushwa ikitokea nchi tajiri inaitwa kashfa, ikitokea nchi masikini inaitwa rushwa,” alisema.
Naye Waziri wa Serikali za Mitaa wa Kenya Musikari Kombo alidai kuwa tatizo kubwa kwa nchi za Afrika ni kuwa fedha zinazopatikana kwa rushwa Afrika hupewa sehemu ya kuhifadhiwa katika nchi tajiri.
Naye Birgit Errath wa Global Compact akiongea nami kwenye mahojiano kuhusu rushwa alisema kuwa dunia inapoteza kiasi cha cha dola zisizopungua trilioni moja kwa mwaka kutokana na rushwa.
Nini hasa dawa ya rushwa?
Sun 11 Sep 2005
Na , Maudhui: Uncategorized
Toa Maoni
Mmoja wa washiriki wa mkutano wa Helsinki, Naeem Mohaiemen, alisema jambo ambalo limekuwa midomoni mwa wajumbe toka alipozungumza. Naeem ambaye ni mtengeneza filamu (
bofya hapa uone moja ya filamu zake)
alidai kuwa wakati ambapo mkutano huu nia yake ni kuunganisha washika dau mbalimbali ili kuweza kujenga demokrasia na usawa sauti za waislamu zimesahaulika. Alisema kuwa kutokana na mtazamo wa watu wengi duniani kuhusu waislamu na uislamu ni vyema waislamu wakahusishwa kikamilifu katika miradi kama hii. Pia alitaka wasanii nao kuhusishwa zaidi kwani wao wana uwezo mkubwa wa kushawishi na kuelimisha umma kutokana na kazi zao.
Sun 11 Sep 2005
Na , Maudhui: Uncategorized
Toa Maoni
Jana nilisahau kuelezea jinsi Watanzania “tulivyowakilisha” kwenye tamasha la kufunga mkutano wa Helsinki. Wakati watumbuizaji kadhaa wa hapa Finland wanafanya vitu vyao, Mama Maria Shaba, mwenyekiti wa Tango,
alikujanje ya ukumbi kutubeba mkikimkiki. Kisa? Alisema lazima Watanzania tukatumbuize. Da! Sauti tunazo? Akasema lazima. Basi Watanzania wote hao jukwaani. Mama Shaba akashika kipaza sauti na kutambulisha kundi la muziki la Tanzania likiongozwa naye akiwa na sauti ya kwanza na Muhidini Issa Michuzi sauti ya nne. Mimi sauti yangu sijui wala ni ya ngapi. Basi tukashusha Malaika nakupenda malaika huku tukijinesuanesua. Ukumbi ukabaki mdomo wazi, waliokuwa mbali wakasogea karibu, mtu wa taa akazitengeneza vyema, zikatumulika. Tukaimba. Tukawakilisha. Tukashangiliwa. Tukafurahi.
Tulipomaliza malaika ikawa sio mwisho. Tukaondoka ukumbini huku tukiimbisha watu wote kiitikio cha wimbo wa Bob Marley wa Get Up Stand Up….Stand Up for Your Rights….come one everybody…Get Up Stand Up….huku tumenyoosha mkono uliokuja ngumi hewani.
Sat 10 Sep 2005
Na , Maudhui: Uncategorized
Toa Maoni
Baada ya wajumbe wa mkutano wa Helsinki 2005 kukubaliana kuwa mwaka 2007, serikali ya Tanzania itaandaa mkutano mwingine kutazama utekelezaji wa maazimio ya mkutano huu….na kuwa kabla ya mwaka huo kamati ndogondogo zitakuwa zikikutana kuratibu juhudi za kufanikisha nia ya kujenga demokrasia na kuondoa umasikini, wajumbe waliagwa kwa tamasha kubwa. Kwanza nilitaka kuacha kwenda mkutanoni maana nilikuwa nimealikwa kwenye harusi moja iliyokuwa inavuma maana ilikuwa inasherehekewa kiafrika na pia nilikuwa nimekaribishwa klabu ya Chelsea kukaa na kujiburudisha na Watanzania wanaoishi hapa Helsinki. Lakini baadaye niliamua kuwa nitakwenda klabu ya Chelsea kisha baadaye niende kwenye tamasha. Na ninasema kuwa sijilaumu kwenda kwenye tamasha.
Kwenye klabu ya Chelsea nilishuhudia mjadala mzito sana sana katika ya wajumbe wa kikao kile, au tuiite kiti moto. Issa Michuzi alikuwa ndio mwenyekiti, akikazana kuzuia wajumbe kupunguza hamasa na kuacha kila mjumbe kumaliza anayotaka kusema. Fide alikaribia kupanda juu ya meza akielezea kuwa mifano tunayotoa ya kusema kuwa nchi kama Malaysia na Singapore zilitawaliwa kama Tanzania lakini zimepiga hatua. Mjadala ulikuwa mpana hasa ukigusia karibu kila jambo kuhusu Watanzania, viongozi wetu, na mfumo wetu wa maisha na utawala.
Kwanini Watanzania tuko nyuma hivi? Lilikuwa swali kuu.
Kulikuwa na mtazamo tofauti kidogo kati ya Watanzania wanaoishi nje na wale waliotokea nyumbani. Sikuongea sana, nilipenda kusikiliza. Baadaye usiku nilifikiri kwa undani yaliyozungumzwa nikagundua kuwa kila lililokuwa linasemwa na pande zote lilikuwa ni sahihi. Ingawa kulikuwa na kutokukubaliana kila mmoja akionyesha mapungufu ya uchambuzi yakinifu wa mwingine, ninaona kuwa wote walikuwa wanasema mambo ambayo yana ukweli ndani yake. Kubwa nadhani ni kutafuta eneo ambalo litaweza kuunganisha mitazamo hiyo ambayo kwa juujuu utaona kuwa inakizana.
Basi baadaye mimi na Michuzi na Vkii wa gazeti la mtandaoni la Malyasiakini la nchini Malaysia tukaenda kwenye tamasha ambapo tulikaa hadi leo asubuhi (Michuzi aliwahi kuondoka) na kuishia kuzunguka mji mzima tukitafuta chakula.
Sisiti kusema kuwa onyesho lile, hasa lile la mpiga kinanda cha mkono (accordian) Kimmo Pohjonen ni kati ya maonyesho ya hisia kali sana ambayo nimetazama karibuni. Mama Maria Shaba wa Tango alichoweza kusema ni kuwa, “Huyu bwana alikuwa anafanya tambiko la kujiponya kama tunavyofanya kule Bwagamoyo kwenye sherehe za kupandisha maruhani. Sisi kwetu tunadharau sanaa kama ile huyu unaona alivyoweza kuteka umati.”
Kumtazama Kimmo ilikuwa ni kama vile kuwa katika ibada fulani hivi. Matumizi yake ya viungo, sauti, kelele, teknolojia, na taa vilinifanya kujisikia kama niko hekaluni.
Namtafuta Mama Shaba nimwambie kuwa aliitaja Bwagamoyo alipokuwa akimzunguzia Kimmo bila kujua. Kwani baada ya onyesho niliongea na Kimmo. Alinishangaza sana alipoanza kuongea nami Kiswahili. Kumbe amesoma muziki wa asili wa Kigogo kule Bwagamoyo na Dodoma. Na alisema kuwa itakuwa ni dhambi asiponiambia kuwa hakuna mtu hapa duniani anayemweshimu kama marehemu Hukwe Zawose. “Muziki wangu na kila kitu nilichokuwa nafanya naweza kusema ni hisia nilizopewa na Zawose.
Fri 9 Sep 2005
Na , Maudhui: Uncategorized
Toa Maoni
Haya, ndio mkutano umefungwa hivyo. mabango yanaondolewa. Viti vinakusanywa. Vitambaba vya mezani vinakujwa. Picha zinapigwa. Anuani kubadilishana. Mvinyo wa mwisho mwisho. Na karanga pia (ila mpishi kazimwagia chumvi kabisa).
Baada ya miezi michache, kutakuwa na mkutano mwingine utakaoitishwa na serikali za Tanzania na Ufini utakaojumuisha washika dau zaidi ambao kazi yake utakuwa ni kuweka mtandao wa kuhakikisha kuwa maazimio ya mkutano huu yanatekelezwa.
Pichani hapo juu ni Watanzania waliokuwa wakishiriki mkutanoni hapa.
Fri 9 Sep 2005
Na , Maudhui: Uncategorized
Toa Maoni
Sisemi kwa ubaya. Ila sidhani kama rais wa Ufaransa, mzee Chirac, alikosea sana alipotoa mawazo yake mwezi wa saba mwaka huu juu ya chakula cha Kifini.
Maneno yake yalikuwa makali kidogo. Jana wakati wa chakula cha usiku, mwandishi mmoja mwandamizi toka Afrika Kusini (amenisihi nisimtaje jina) aliniambia, “Kwetu bwana Macha ukila chakula hiki unakuwa ni sawa tu na mtu aliyelala njaa.”
Nikamwambia, “Mbona?”
Akashangaa, “Yaani wewe huoni? Kwani hiki ni chakula? Unajua wajumbe toka India kila siku wanajipikia wenyewe kwa zamu kule jikoni.”
Tuache chakula chao, Finland kama hufahamu ni nchi ambayo utenzi uliisaidia ikapata uhuru. Huu ni ule utenzi wa Kalevala.
Mwaka 2000 nilishuhudia kundi la Parapanda likiigiza utenzi huu katika juma la makumbusho pale Dasalama. Kaiti ya mambo ambayo nchi hii inajivunia ni kazi za mchora ramani za majengo wa Kifini, Alvaro Aalto. Jengo la Finlandia Hall ambamo mkutano wa Helsinki unafanyika limechorwa na huyu bwana.
Katika mazungumzo na watu mbalimbali kumezuka mjadala kuhusu nchi za Afrika kusemekana kuwa ziko nyuma kimaendeleo kwakuwa zilitawaliwa. Swali hili limeulizwa: iweje Finland iliyotawaliwa karibu miaka 700 na Waswidi na miaka 150 na Warusi iwe mbele namna hii kiuchumi na kijamii?
Elimu na afya katika nchi hii hutoi hata sumni. Tofauti na nchi ya kibeberu kama Marekani, Finland hakuna shule au vyuo vikuu vya binafsi/kulipia.
Fri 9 Sep 2005
Na , Maudhui: Uncategorized
Toa Maoni
Katibu Mkuu wa shirika la kutetea haki za binadamu, Amnesty International,
Irene Khan,
akiongea hapa Helsinki jana, alisema kuwa vita dhidi ya ugaidi vimekuwa ni kisingizio cha baadhi ya nchi duniani kutupilia mbali haki za msingi za binadamu.
Akizungumzia kuhusu vita duniani alisema kuwa silaha ndogo ndogo, ambazo ndio zinazotumika katika vita sehemu mbalimbali duniani, ndio hasa silaha za maangamizi. Mataifa makubwa yanayopata faida kubwa kutokana na biashara ya silaha hizo lazima yabanwe ili kuacha biashara hiyo chafu. Zaidi ya watu nusu milioni huuliwa na silaha ndogondogo kila mwaka.
Alimaliza kwa kutuambia kuwa idadi ya risasi zilizoko duniani ni kubwa mno kwani kuna risasi mbili kwa kila binadamu hapa duniani.
Thu 8 Sep 2005
Na , Maudhui: Uncategorized
Toa Maoni

Mpiga picha maarufu wa gazeti la Daily News Tanzania, Muhidin Issa Michuzi amekata shauri. Hajakata shauri kumpokea bwana, bali kuwa mwanablogu wa picha (photoblogger). Basi kuanzia leo umtembelee. Ninakuhakikishia kuwa hutajilaumu. Picha zake nimekuwa nazipenda toka zamani. Tumekutana hapa Helsinki. Bofya hapa umtembelee na kumkaribisha.
Kwenye picha hii tuko kwenye tafrija fupi ys kumkaribisha kwenye uwanja wa blogu.
Thu 8 Sep 2005
Na , Maudhui: Uncategorized
Toa Maoni

Wanaharakati Philipina, Halima, Felista Rugambwa, na Angel Damas tukitazama onyesho la “man free yourself!” ndani ya jengo la Finlandia Hall.
** Picha na Muhidin Issa Michuzi.
Thu 8 Sep 2005
Na , Maudhui: Uncategorized
Toa Maoni

Muhidin Issa Michuzi kamaliza kutuchukua picha hii. Hawa wote ni Watanzania wanaohudhuria mkutano hapa Helsinki.
Kutoka kushoto ni ndesanjo mwenyewe, Abubakar Rajab ambaye ni katibu mkuu wizara ya kazi na maendeleo ya vijana, Philipina Labia wa shirika la Faraja Human Development Trust Dodoma na mjumbe wa bodi ya TANGO,
Halima Zinga wa Chama cha Elimu ya Watu Wazima Tanzania, Angel Damas wa Youth of the United Nation Association (ambaye ndiye miss Tanzania 2005), Abdulkader Shareef (Naibu Waziri, wizara ya mambo ya nje), Felista Rugambwa wa Youth of the United Nations Association (ambaye ni Miss University 2005), anayefuata nitatafuta jina lake, Omary Mjenga wa wizara ya mambo ya nje, na Robert Kahedaguza toka wizara ya mambo ya nje, anayefuata nimemsahau jina ila katoka maendeleo ya jamii
Thu 8 Sep 2005
Na , Maudhui: Uncategorized
Toa Maoni

Marais Benjamin Mkapa wa Tanzania na Tarja Halonen wa Ufini wakiongea asubuhi hii. Marais hawa wamesisitiza kuwa muundo wa kisiasa na kiuchumi duniani unahitaji kubadilishwa. Mkutano wa Helsinki ni hatua muhimu katika kutafuta namna ya kujenga duniani ambayo inajali utu na haki za msingi za binadamu. Umuhimu wake unatokana na ushirikishwaji wa washikadau wa sekta mbalimbali.
Thu 8 Sep 2005
Na , Maudhui: Uncategorized
Toa Maoni
Mama Maria Shaba, mwenyekiti wa Tanzania Association of Non-Governmental Organizations (TANGO), aliongea jana wakati wa mjadala kuhusu wanawake na maendeleo. Alisema kuwa kuna umuhimu wa kubadili tafsiri ya umasikin. Alionya kuwa Waafrika wanatakiwa kuwa makini sana kutokana na vyombo vya habari/uongo vya magharibi kusema kila mara kuwa sisi ni masikini. Unapoambiwa kuwa wewe ni masikini kila kukicha mwishowe unaamini kabisa kuwa wewe ni masikini hata kama ukweli ni kuwa wewe ni tajiri.
Akauliza kama sisi ni masikini kwanini mabepari wamekazana kuwekeza Afrika? Kwanini makampuni yao yanapeleka huduma na bidhaa zake kwa waafrika? Na kama ni kweli kuwa sisi ni masikini kiasi ambacho hata fedha wanazodai kutukopesha hatuwezi kulipa kwanini basi wanaendelea kutukopa kila siku??
Hivi sasa kuna kwaya moja inatumbuiza. Kumbe Wafini wanajua kuimba kama wagogo?
— Next Page »