June 2007
Monthly Archive
Thu 28 Jun 2007
Ukimya utamalizika nitakapowasili kwa Joji Kichaka toka kijijini. Habari za kuandika ni nyingi. Soma Gumzo la Wiki jumapili kwenye gazeti la Mwananchi kwa habari nilizoandika nikiwa Tanzania.
Usisahau kuwa uchaguzi wa viongozi wa Jumuiya ya Wanablogu Tanzania ni tarehe 29 na 30 Juni mwaka huu. Bonyeza hapa ujue jinsi ya kupiga kura katika siku hizo mbili.
Wed 13 Jun 2007
Na Ndesanjo Macha, Maudhui:
mseto ,
tanzaniaToa Maoni [6]
Kama huijui blogu ya BongoCelebrity sijui unasubiri nini. Hutajilaumu kuwa umepoteza muda ukiitembelea. Ni blogu (tovuti?) yenye habari za kujenga kuhusu watu mashuhuri. Sio habari za kubomoa ambazo ndio hasa huonekana kuwa zinauza zinapoandikwa magazetini. Blogu hii inawatazama watu mashuhuri kwa jicho chanya na kuongea nao ili tuweze kujifunza toka kwao. Heko wana BongoCelebrity. Huku ndio kukomaa kwa Watanzania mtandaoni. Wenyewe wanajielezea hivi:
Karibu ndani ya BongoCelebrity. Hii ni tovuti/blog ambayo inaandika kuhusu watu mashuhuri au maarufu wa Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla. Tunaandika na kujadili habari za watu mashuhuri wa zamani na wa sasa hivi. Nia ya msingi ni kujenga na sio kubomoa.Tupende tusipende, maisha ya watu maarufu (celebrities) yana mvuto mkubwa kwa jamii.
Bonyeza hapa uwatembelee.
—
KUNIPATA MOSHI KWENYE SIMU, PIGA: O171-368-585 0717 368-585
Mon 11 Jun 2007
Uchaguzi wa jumuiya yetu utakuwa mzuri sana. Naamini watu watakaochaguliwa wataweza kutuongoza kuwa jumuiya imara na yenye mwelekeo wa kimaendeleo. Kila aliyejitokeza kugombea anaelekea kufaa. Sijui tutamchagua nani na kumwacha nani. Kuna kazi. Bonyeza hapa utembelee blogu yetu ili uone wanaogombea nafasi za uongozi (swali na “ndesanjo, mbona hugombei?,” nitalijibu mbeleni).
Napenda pia kuwakumbusha kuwa tarehe ya mwisho ya kuomba fedha za miradi ya uandishi wa rais, Rising Voices, toka Global Voices Online ni tarehe 15 mwezi huu. Nilisema kuwa wanaoomba kama watapenda kushauriana nami, wasisite kuniandikia. Ukishindwa kutuma maombi safari hii usiwe na tabu kwani kabla ya mwaka kuisha awamu ya pili ya fedha hizi itatolewa. Soma hapa kuhusu Rising Voices.
—–
Habari za Moshi ni salama. Tumetulia tu. Nimeambiwa eti nikae macho nisifanywe “ATM” na mabinti wana mji! Nisipigwe na changa la macho.
Thu 7 Jun 2007
Na Ndesanjo Macha, Maudhui:
mseto ,
afrika ,
mikutanoToa Maoni [8]
Mapema leo Kikwete aliongea na wana TEDGlobal 2007. Soma aliyosema toka kwa Ethan Zuckerman (kiingereza) na Sankofa (Kiswahili)
Wakati nafurahia tangazo la Waafrika 100 waliopewa skolashipu watapewa kompyuta mpya za mapajani za bure, nimepata habari nyingine ya kufurahisha. Mkurugenzi wa Google, Larry Brilliant, kaniambia kuwa atafanya kila awezalo ili wanablogu wa Afrika waweze kukutana barani Afrika.
Wafanyabiashara hawana Kiswahili kirefu. Nilipomgusia suala hilo, ameuliza maswali matatu: Watu wangapi wanatakiwa kuhuduria, utafanyika wapi, na gharama yake ni kiasi gani. Uzuri ni kuwa jana wanablogu kadhaa tulikutana kujadili suala hili hivyo nilikuwa na uwezo kiasi fulani wa kujibu maswali hayo.
Wanablogu tumekuwa tunakutana sana, ila tunakutana kwenye mikutano ya watu wengine. Kuna kila sababu ya sisi wanablogu kukutana kwenye mkutano wetu, kujuana, kujadili, kubadilishana mawazo, ushauri, n.k.
Thu 7 Jun 2007
Na Ndesanjo Macha, Maudhui:
msetoToa Maoni [1]
Rais Kikwete amemaliza kuongea na wanaohudhuria mkutano huu wa TEDGlobal 2007. Nimekaa ndani ya chumba ambacho Kikwete atakuja kufanya mahojiano na waandishi wa habari na wanablogu.
* Leo tumeambiwa kuwa watu wote 100 (wakiwemo Watanzania kadhaa) waliopewa skolashipu za kuja kwenye mkutano huu watapewa kompyuta mpya (PC au Mac) toka kwa Google na MAD.
Wed 6 Jun 2007
Na Ndesanjo Macha, Maudhui:
Muziki ,
mikutanoToa Maoni [1]
Vusi kamaliza shoo yake muda mfupi uliopita. Soma hapo chini niliyoweza kuandika katikati ya kuingia na kiwewe cha furaha ya kuona jabali hili la muziki wa Kizulu.
—-
Vusi anasema ametoka Mamelodi Township. Kisha anafafanua, “Township is a ship going to town but never get there.”
Wimbo wake wa pili alioimba ni kati ya nyimbo zake ninazozipenda mno. Ndio wimbo kwenye video niliyowawekea hapo awali. Kama hujaiona, bonyeza hapa.
Anasema:
Who died last night
Who died this morning
And why?
Skeletons confessing
The age of lamentation
Alipomaliza wimbo huu aliamua kutuni gitaa lake. Akatuingiza mjini kwa kusema, “Wimbo ufuatao ni wimbo wa Kichina.” Eti wimbo wenyewe unaitwa “tuning.” Kumbe alikuwa anarekebisha nyuzi za gitaa lake. (more…)
Wed 6 Jun 2007
Na Ndesanjo Macha, Maudhui:
Muziki ,
mikutanoToa Maoni
Jukwaani anaingia mmoja wa wanamuziki, washairi, na wanaharakati wakubwa na ninaowapenda…Vusi Mahlasela. Mtazame kwenye video hii…wakati unamtazama kwenye video sisi tunamtazama moja kwa moja.
Wed 6 Jun 2007
Na Ndesanjo Macha, Maudhui:
filamu ,
afrika ,
mikutanoToa Maoni
Franco Sacchi anaanza kwa kusema, “Habari ya jioni.”
Kwanza kulikuwa na Hollywood, ikaja Bollywood (India), na sasa Nollywood. [maneno yangu: pia kuna Lollywood]
Mwaka 2006 karibu filamu 2000 zilitengenezwa nchini Nigeria. Inakadiriwa kuwa filamu za Nollywood zinafikia kiasi cha dola milioni 250 na maelfu ya watu wamepewa ajira kutokana na filamu hizi.
Unajiuliza, inakuwaje mtengeneza filamu wa Kiitalia anayeishi Boston anafuatilia filamu za Afrika. Jibu ni hili: babu yangu aliishi Zambia, baba yangu pia, nami nilizaliwa Zambia.
Afrika inachukuliwa kwa njia mbili: mtazamo wa kitalii na mtazamo wa vyombo vya habari (njaa, vita, magonjwa). Aliamua kuanza kueleza habari kuhusu Waafrika wanaotengeneza filamu. Akatengeneza filamu kuhusu filamu Afrika. Katika kutengeneza filamu hiyo, walikwenda Lagos kukutana na mmoja wa watengeneza filamu wa Nigeria (sina sijalipata vizuri). Walichofanya ni kumfuatilia ndugu huyu akitengeneza filamu iitwayo Check Point.
Anatuonyesha sehemu ya filamu yake….[maneno hapo chini ni baadhi ya nukuu toka kwenye sehemu hii ya filamu yake]
- unaweza tengeneza filamu kwa dola elfu kumi tu za Kimarekani kwa muda wa siku saba
- filamu zetu sio za gharama kubwa, unatengeneza filamu moja haraka, ukimaliza unatengeneza nyingine la sivyo utakufa njaa
- kwa sasa hatuangalii ubora, ubora utakuja baadaye. Kumbuka Afrika imejaa watu wanaoishi kwa chini ya dola moja kwa siku
- Hakuna mtu aliyeamini kuwa Nollywood ingetokea Afrika
- Watu wanapenda filamu hizi maana visa vyenyewe ni sawa na visa kwenye maisha yao
- Tutakuja kufanya kitu ambapo dunia ikiona itashangaa
- Niligundua kuwa naweza kufanikiwa bila kuiba au kudanganya…kwa kutumia kipaji alichonipa mungu
Franco anaendelea: Teknolojia za dijitali zimesaidia kupunguza gharama ya kutengeneza filamu. Wanigeria wamechukua teknolojia hii na wanaitumia kwa mafanikio makubwa. Nchi nyingine za Afrika zinatakiwa kujifunza toka Nigeria na kuanza kutengeneza filamu na katika kufanya hivyo, watakuwa wanazalisha ajira.
Nawapeni changamoto: fikiria dunia ambayo ina chakula, mavazi, na malazi ila hakuna hadithi, visa, fasihi, n.k. Itakuwa dunia ya ovyo.
Anatuonyesha sehemu nyingine ya filamu yake…
- naamini muda sio mrefu tutakuwa na filamu bora zaidi
- tunatengeneza filamu hizi kwa kufuata mantiki na mazingira ya Nigeria
Franco anashukuru waandaaji wa mkutano huu, TEDGlobal 2007, kumpa nafasi ya kuwa balozi wa filamu za Nollywood.
Wed 6 Jun 2007
Nik Nesbitt ni mwanzilishi wa kampuni ya KenCall. Anazungumzia jinsi ambavyo tunaweza kubadili sura ya Afrika. Toka Afrika ya matatizo kuwa Afrika ya ustawi. Anatuonyesha picha mbalimbali zinazotumika kuonyesha sura ya Afrika (picha nyingi huwa kama si za watu wanaokufa njaa basi zitakuwa picha za wanyama). Anaonyesha picha ya Mlima Kilimanjaro (na kugusia tishio la kuyeyuka kwa barafu. Anaonyesha picha nyingine ya watalii wakitazama piramidi. Anasema picha hii haionyeshi watu wa Afrika wamefanya nini miaka ya karibuni [kwani piramidi zilitengenezwa miaka mingi iliyopita]. Picha nyingine ya Twiga katika mbuga ya wanyama anayosema kuwa inaonyesha Afrika iliyotulia na isiyo na kelele zaidi ya nyimbo za ndege. (more…)
Wed 6 Jun 2007
Na Ndesanjo Macha, Maudhui:
msetoToa Maoni
Tunatumbuizwa na kundi la Zip Zap. Zip Zap ni shule ya sarakasi iliyoko nchini Afrika Kusini. Wamewachukua wahudhuriaji wawili na kuwapandisha jukwaani kisha wanawafanya wafanye mambo kadhaa ya kuchekesha kama kucheza, kuendesha gari hewa, n.k. (more…)
Wed 6 Jun 2007
Na Ndesanjo Macha, Maudhui:
blogu ,
mikutanoToa Maoni [1]
Nimechelewa kufika mkutanoni leo. Niliamka alfajiri na mapema kwenda Moshi. Hivyo nimekosa mengi yaliyozungumzwa asubuhi na mchana. Ila kwakuwa wapo wanablogu wengi wanaohudhuria mkutano huu, nitaweza kujua yaliyoendelea.
Kati ya blogu hizo ni Mwenye Macho.
Jana usiku, mmoja wa wasomaji wa blogu wa muda mrefu, mtengeneza filamu na mpiga picha Sankofa, alifungua blogu yake: Mwenye Macho. Ninavyomfahamu Sankofa na kamera yake, blogu hii itakuwa na sura na mchango wa aina yake. Itembelee blogu ya Mwenye Macho uone picha mbalimbali za matukio ya mkutano wa TEDGlobal 2007.
Tue 5 Jun 2007
Segeni wa Mamamikes toka Kenya ni wale jamaa poa sana. Basi jana alipewa dakika tatu kuongelea Mamamikes. Teknolojia mpya imetuletea biashara mpya kama ya Mamamikes. Sasa dakika hizo tatu alizitumia kwa kutuonyesha video ambayo kwa muda mfupi inakueleza Mamamikes ni nini. Bonyeza hapa utazame video yenyewe uifahamu Mamamikes.
Tue 5 Jun 2007
Na Ndesanjo Macha, Maudhui:
mikutanoToa Maoni
Jane Godall anaanza kuwa kusema kuwa tunaweza kusalimiana kwa lugha mbalimbali za wanadamu, lakini pia tunaweza kusalimiana kwa..….anatoa mlio wa Sokwe wanaotumia kuwasiliana. Anasema sokwe ndio wenye tabia zinazofanana nasi kuliko mnyama yoyote yule.
Sokwe huishi hadi miaka 60 hadi zaidi. Sokwe huzaa akiwa na miaka 11 au 12 na baadaye kuendelea kuzaa kila baada ya miaka mitano au sita. Watoto wa Sokwe hulala na mama zao, mama zao huwabeba, n.k. (more…)
Tue 5 Jun 2007
Na Ndesanjo Macha, Maudhui:
Muziki ,
mikutanoToa Maoni [1]
Ukumbi ulimwagika kwa makofi na kelele baada ya Bi Kidude kuingia ukumbini na kutusalimu kwa mikono yake. Makofi, baadhi ya watu wakasimama (ile wazungu wanaita “standing ovation”). Nami nikajazia kwa zile mbinja nilizokuwa napiga nikiwa mdogo kuitana na washikaji kwenda kucheza.
Anaimba huku akikung’uta msondo. Anasindikizwa na wapiga ngoma wengine wawili na wasichana wachezaji na waitikiaji watano. Wanaokata viuno. Kata kiuno, kata. Kata kiuno, kata. Kiuno chako mwenyewe… (more…)
Tue 5 Jun 2007
Na Ndesanjo Macha, Maudhui:
teknolojia ,
afrikaToa Maoni
Simon Mwacharo, Mkurugenzi Mkuu wa Craftskillz, amepewa dakika chache aongelee mradi wake wa kutengeneza mashine za kuzalisha nishati mbadala Afrika. Anasema Afrika inategemea chanzo kimoja tu cha nishati jambo ambalo linabidi kubadilishwa kwa kubadili sera za nishati na kuanza kutumia teknolojia mpya.
Simon anafanya kazi katika mradi unaozalisha nishati kwa kutumia jua na upepo. Anasema kuwa Mkenya anatumia kama shilingi 100 ya Kenya kwenda kwenye nyumba yenye nishati ili kuchaji simu yake ya kiganja. Asilimia 85 ya Wakenya wako kwenye maeneo yasiyo na nishati ya umeme. (more…)
Tue 5 Jun 2007
Ted Kinadae toka Ethiopia anatoa mada hii: Flattening Wireless Messaging (SMS and IM mobile messaging with no boundary). Kampuni yake yake inaitwa Feedlix. Tovuti ya kampuni hii inasema hivi kuhusu huduma zake: FeedeliX Wireless Inc. is California based company specializing in providing mobile text and instant messaging solutions for users of Latin as well as major Non-Latin scripts such as Hindi and Ethiopic based on a proprietary technology. (more…)
Tue 5 Jun 2007
Na Ndesanjo Macha, Maudhui:
teknolojia ,
afrika ,
mikutanoToa Maoni
Ainea Kimaro wa mradi wa Biogas and Solar wa Tanzania amepewa dakika tatu kuongea. Anaongelea mada hii: Organic Waste - the ignored resource. Anachoongelea ni haja kubwa! Anasema kuwa nchi zenye mafuta ziko mbalil, kwanini tusitumie nishati ambayo imetuzunguka.
Anatuonyesha jinsi ambavyo wanatumia teknolojia rahisi ili kuzalisha nishati kwa kutumia kinyesi cha mwanadamu. Mradi huu unazalisha nishati kwenye mashule, magereza, n.k.
Haya, dili ya kinyesi!
Tue 5 Jun 2007
Na Ndesanjo Macha, Maudhui:
Muziki ,
mikutanoToa Maoni [1]
Ratiba inaonyesha kuwa baadaye leo kutakuwa na onyesho la gwiji wa muziki bara la Afrika na dunia muzima, Fatuma Binti Baraka, maarufu kwa jina la Bi Kidude.
Tue 5 Jun 2007
Na Ndesanjo Macha, Maudhui:
teknolojia ,
afrika ,
mikutanoToa Maoni
Florence Seriki aliyeko jukwaani ni mwanzilishi wa kampuni ya kutengeneza kompyuta, Omatek, ya nchini Nigeria. Anasema kuwa lazima Waafrika tujiulize ni vipi tutaweza kujifunza toka kwa nchi kama China.
- Alivyoanza kujihusisha na masuala ya kompyuta: alisoma kemia, lakini wakati fulani akawa anahitaji kutumia kompyuta ili kufanya uchambuzi wa kemikali. Kwakuwa hawakuwa na kompyuta ilimbidi atafute vipuri vya kompyuta na kuunda kompyuta yake.
- Ni rahisi sana kufanya mambo makubwa Afrika maana Waafrika tunajua sana kuvumulia.
- Jina la kampuni yake, Omatek, ni jina la kijiji chake.
- Alijifunza mengi toka kwa Wachina. Wachina hawatumii benki za nje, wanatumia benki za Kichina.
- Alianzisha kampuni yake mwaka 1992
- Alipata Tuzo ya Kwame Nkrumah mwaka 2005
- Usiseme kwakuwa wewe ni Mwafrika basi huwezi kufanya kama wanavyofanya Wachina
- benki za Afrika zinahitaji kutoa mikopo ili kusaidia wafanyabiashara wadogo.
- Watu wengi katika sekta ya kibinfsi waanze kunua bidhaaa toka ndani
- Anasema kuwa changamoto sasa ni kuingia kwenye hatua mpya, toka kwenye kutengeneza kompyuta na kuanza kubuni na kusanifu kumpyuta.
Tue 5 Jun 2007
Na Ndesanjo Macha, Maudhui:
Muziki ,
mikutanoToa Maoni [1]
Dakika hii jukwaani yupo mwanamuziki Abenaa. Abenaa ni mzaliwa wa baba Mghana na Mama toka Trinidad. Anaishi New York, Marekani. Jina lake, Abenaa, ni jina toka Ghana linalomaanisha kuwa alizaliwa siku ya jumanne. Ndio maana albamu yake inaitwa Tuesday’s Child. Yuko jukwaani na wanamuziki wengine wawili, mmoja anapiga gitaa na mwingine anapiga ngoma. Ajabu ni kuwa anayepiga ngoma wamekutana naye leo! Huyu ni ndugu aitwaye Freddy ambaye ni mtanzania. Nitamtafuta Freddy baadaye kujua kama ni mwanamuziki au la. Anapiga ngoma kama vile amekuwa ni mwanamuziki wa Abenaa kwa muda mrefu. Ila wanamuziki ndivyo walivyo. Wako tayari saa yoyote. Kama askari wanavyotakiwa wawe. Dakika yoyote.
Watu wengi wamehuzunika kusikia kuwa Yossou Ndour hataweza kuhudhuria mkutano na kutumbuiza kutokana na matatizo fulani ya kibinafsi.
—-
*Alhamisi kutakuwa na mgeni wa kushtukiza kwenye mkutano huu. Sitakiwi kutamtaja. Subiri.
— Next Page »