Mjadala ulikuja, ukapita. Wana Jikomboe wa New York walinipokea vizuri. Shukrani. Balozi wa Sudani alikuwemo, kinyume na taarifa kuwa asingetokea. Wakajadili. Tukasikiliza. Ikapita. Darfur, damu na machozi vinamwagika.

Nilidhani kungekuwa na wanablogu wengine, hasa wale wanaoandika masuala ya siasa ambao wamejaa New York. Hapana, nadhani ingekuwa Washington DC wangekuwemo. Mwanablogu mwingine aliyehudhuria ni Rebecca MacKinnon, mmoja wa waanzilishi wa Global Voices Online na mwalimu wa uandishi wa habari wa mtandaoni Chuo Kikuu Cha Hong Kong.

Balozi wa Sudani sikummaliza. Alionekana kushangazwa sana na watu wanaodai kuwa hali Darfur ni mbaya sana. Hoja yake ni kuwa kiburi na vitisho vya Marekani ndio vinawapa vichwa Janjaweed. Anasema pia idadi ya watu ambao wameuawa ni ndogo zaidi ya ile inayotajwa kwenye vyombo vya habari. Kuna uchambuzi umeandikwa na mwanablogu wa Sudan, Sudanese Thinker ambaye ni mwanzilishi wa blogu ya We Blog for Darfur. Msome.
——-
Hivi blogu zina nafasi gani katika harakati dhidi ya mauaji ya watu wasio na hatia kama inavyotokea Darfur? Niliandika makala fupi kuhusu suala hili kwenye ukurasa wa Global Voices. Iliitwa, Sudan: Blogging From the Conflict Zone. Isome uone jinsi gani blogu zinavyotuwezesha kushiriki kwenye harakati na utetezi kwa njia mpya.