Katika mijadala mtandaoni ninayoifuatilia kwa karibu ni ile inayotazama jinsi gani uandishi wa raia unafanya kazi. Je kuna matatizo gani yanayoletwa na uandishi huu? Kuna mapungufu gani? Kuna mazuri yapi? Nini sisi wanablogu tunapaswa kujifunza na kuboresha? Je uandishi huu unaipeleka wapi jamii? Na mambo kama hayo. Dhana hii inanigusa na hata wakati mwingine huwa naiota.

Basi mwezi uliopita kulilipuka bomu kwenye kituo cha basi nchini Kenya. Wakati tovuti za magazeti makubwa ya Kenya, Daily Nation na East Africa Standard, walikuwa hawana habari hizo. Tayari wanablogu walishazitoa na hata kuweka picha na kuendelea kutoa habari kila zinazowafikia. Hili ni jambo ambalo sisi tunatangaza injili hii ya uandishi wa raia na mapinduzi ya blogu linatufanya tutabasamu. Lakini…kulikuwa na walakini. Au hakukuwa na walakini kutegemea utakuwa umelalia upande gani. Upande wa mjadala mkali na mzuri ambao ulitokana na mambo aliyoandika Mental Acrobatics na Thinkers Room, kati ya wanablogu wakubwa na wa muda mrefu nchini Kenya.

Sasa ili ujue hasa mjadala wenyewe, soma makala niliyoandika iliyochapwa pale GV (Global Voices Online). Bonyeza hapa.